Kauli ya Pinda yaonyesha udhaifu’
Baadhi ya wanasiasa na wanaharakati wamemkosoa Waziri Mkuu,
Mizengo Pinda kutokana na kutamani kung’olewa kwenye nafasi, wakidai
kuwa kauli yake inaonyesha jinsi alivyo mpole na dhaifu kiutendaji .
Mkurugenzi wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu
(LHRC), Dk Hellen Kijo-Bisimba ayezungumza na gazeti hili jana kwa njia
ya simu alisema kuwa kauli ya Waziri Mkuu Pinda imeonyesha kwamba ana
tatizo la kutokujiamini.
“Kazi za Waziri Mkuu zinajulikana wazi kwamba ni majukumu mazito
ikiwemo kusimamia utendaji wa Serikali kwa kila wizara, hivyo kusema
asihukumiwe kwa sababu ya wizara chache zisizofanya vizuri, inaonyesha
ameshindwa majukumu yake. Alichotakiwa kufanya kwa wizara hizo ni
kumshauri Rais awaondoe madarakani wasiowajibika,” alisema.
Alisisitiza: “ Hatutegemei kumwona Waziri Mkuu
akiingia kufanya kazi kwenye kila wizara, isipokuwa anatakiwa kumshauri
Rais ili mambo yaende sawa.” Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Wananchi (CUF), Julius
Mtatiro, alisema kuwa amekuwa akifuatilia kauli za Waziri Mkuu Pinda
hata anapokuwa kwenye ziara za kikazi, ambapo amekuwa akitoa kauli za
kuwabembeleza watendaji, hata wanapoboronga.

Familia ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere itawakilishwa katika mazishi ya Rais wa Kwanza Mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, ambaye atazikwa kesho katika Kijiji cha Qunu, Mthatha Jimbo la Eastern Cape.
Familia ya Nyerere yaenda Qunu kumzika Mandela

Familia ya Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere itawakilishwa katika mazishi ya Rais wa Kwanza Mzalendo wa Afrika Kusini, Nelson Mandela, ambaye atazikwa kesho katika Kijiji cha Qunu, Mthatha Jimbo la Eastern Cape.
Habari ambazo gazeti hili lilizipata jana mjini
Pretoria zinasema kuwa Mama Maria Nyerere, ambaye ni mjane wa Baba wa
taifa, alialikwa kuhudhuria mazishi hayo kwa kuzingatia uhusiano uliopo
baina ya familia hizo mbili.
Hata hivyo, imethibitika kuwa Mama Maria hataweza
kuhudhuria mazishi hayo kesho, badala yake amewatuma wawakilishi ambao
ni mabinti zake wawili; Anna Nyerere ambaye ni mtoto wa pili na mtoto
wake wa saba, Rosemary Nyerere.
Madaraka Nyerere ambaye ni mtoto wa sita wa Mwalimu
alithibitisha jana kwamba familia yao imealikwa kushiriki mazishi hayo,
lakini akaweka wazi kwamba: “Mama hataweza kwenda kuzika, atakwenda
baadaye kidogo baada ya mazishi kufanyika.”
Madaraka alisema kwa jinsi afya ya mama yake
ilivyo sasa, hataweza kwenda Qunu. “Kwa kawaida mazishi haya ya kitaifa
huwa yana mambo na pilika nyingi, kwa hiyo mama ameona asubiri,”
alisema.
Dk Kawambwa ajibu makombora ya Nape
Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk Shukuru Kawambwa
amejibu madai yaliyotolewa hivi karibuni na Katibu wa Itikadi na Uenezi
wa CCM, Nape Nnauye kwamba ni mmoja wa mawaziri walioshindwa kazi, hivyo
kustahili kung’olewa.
Katika madai yake, Nape alisema Dk Kawambwa
ameshindwa kusimamia vyema madai ya walimu na kwamba akiwa Waziri wa
Miundombinu, aliingia mkataba na Kampuni ya ujenzi ya Progressive
iliyopewa zabuni ya kujenga Barabara ya Namtumbo hadi Tunduru wakati
mkandarasi huyo hana uwezo wa kuijenga.
Nape alikaririwa akisema kwamba umefika wakati kwa
waziri huyo na wenzake wa Fedha, Dk William Mgimwa; Kilimo, Chakula na
Ushirika, Christopher Chiza; na Naibu wake, Adam Malima kuhojiwa na
Kamati Kuu (CC) ya chama hicho.
Kairuki ataka ushirikiano kuukabili unyanyasaji
Washiriki mbalimbali wa maendeleo na wadau wa masuala ya jinsia wametakiwa kushirikiana na Serikali katika kuhakikisha vitendo vya ukatili na unyanyasaji wa kijinsia vinafikia tamati.
Rai hiyo imetolewa jijini Dar es salaam na Naibu
Waziri wa Katiba na Sheria, Angellah Kairuki wakati akizindua siku 16 za
kupinga ukatili na unyanyasaji wa kijinsia.
Sambamba na uzinduzi huo Kairuki alizindua pia
mfumo wa utoaji wa huduma kwa mfumo wa One Stop Center ambao unajumuisha
huduma zote muhimu kwa watakaokutana na ukatili wa kijinsia kama vile
polisi, afya na ustawi wa jamii kutolewa sehemu moja.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni