Jumatano, 27 Novemba 2013

Chadema yasema Zitto aliponzwa na waraka tu


Chama cha Demokrasia na Maendeleo, Chadema kimesema kwamba kilifikia uamuzi wa kumvua nyadhifa zake, aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wake, Zitto Kabwe kutokana na sababu moja tu ya kuhusika katika Waraka wa Mkakati wa Mabadiliko 2013.
Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu aliwaambia waandishi wa habari Dar es Salaam jana kwamba waraka huo unaeleza mbinu za uasi ambazo zililenga kufanya mabadiliko makubwa ya kiuongozi wakati wa uchaguzi mkuu wa ndani wa chama hicho jambo ambalo ni kinyume na katiba, sheria na itifaki za Chadema.
Hivi karibuni, Kamati Kuu ya Chadema iliwavua nyadhifa zao, Zitto, Mjumbe wa Kamati Kuu, Dk Kitila Mkumbo na Mwenyekiti wa Mkoa wa Arusha, Samson Mwigamba kutokana na madai hayo.
Siku tatu zilizopita, Zitto na Dk Kitila waliitisha mkutano wa wanahabari na kueleza sababu mbalimbali za kung’olewa kwao ikiwamo suala la posho na ruzuku za vyama vya siasa.


Polisi yapiga marufuku kuuza visu, sime, mapanga barabarani

 
Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, imepiga marufuku biashara ya kutembeza visu, sime na mapanga barabarani na kusema yeyote atakayekiuka agizo hilo atakamatwa na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Kanda hiyo, Kamishna Suleiman Kova alisema jeshi hilo lipo katika mchakato wa kupendekeza sheria mpya ya matumizi ya silaha na umiliki ili kudhibiti matumizi mabaya yakiwamo uuzaji wa visu, mapanga na sime kiholela.
Kamishna Kova alisema tatizo kubwa si mtu kumiliki silaha, bali jinsi watu wanavyozitumia vibaya na kusababisha madhara katika jamii na kuongeza kuwa sheria hiyo itajumuisha uuzaji holela wa visu, mapanga na sime barabarani na umiliki wa silaha za  moto.



Tume ya Sheria ‘yalilia’ mapendekezo yake

 
Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, imepeleka mapendekezo ya kuboresha sheria 32 serikalini tangu ilipoanzishwa mwaka 1983, lakini zilizofanyiwa kazi ni 13.
Akitangaza maadhimisho ya miaka 30 tangu kuanzishwa kwa tume hiyo jana, Mwenyekiti wa Tume ya Kurekebisha Sheria Tanzania, Jaji Aloysius Mujulizi alisema hiyo ni changamoto kwao kwa sababu tume haina kipengele cha sheria kinachoiruhusu kuhoji Serikali kama mapendekezo yake hayajafanyiwa kazi. Jaji Mujulizi alisema miongoni mwa kazi za tume hiyo ni kufanya mapitio ya sheria na kupendekeza, ili zifanyiwe marekebisho kulingana na mahitaji ya watu na wakati uliopo.
Alizitaja baadhi ya sheria zilizotungwa kutokana na kazi ya Tume hiyo kuwa ni, Sheria ya Kazi ya mwaka 2004 na Sheria ya Mtoto ya mwaka 2009.
 Nyingine ni Sheria ya Usimamizi wa Vinasaba vya Binadamu ya mwaka 2009 na kutungwa kwa kanuni mpya za Mahakama ya Rufaa ya mwaka 2009.
Jaji Mujulizi alisema kazi nyingine zinazofanywa na tume hiyo ni kufanya tafsiri za sheria mbalimbali kutoka lugha ya Kiingereza kwenda Kiswahili.
“Kutokujua sheria haiwezi kuwa kinga kwa anayeivunja, hivyo tumekuwa tukitafsiri sheria mbalimbali ili wananchi waweze kuwa na uelewa na hivyo kuzifuata,” alisema.
Alitaja baadhi ya sheria zilizotafsiriwa kuwa ni Sheria ya Mikataba, Sheria ya Ajira na Uhusiano Kazini, Sheria ya Kuzuia Fedha Haramu na Sheria ya Usimamizi wa Mirathi.
Kuhusu maadhimisho hayo, Jaji Mujulizi alisema Rais Jakaya Kikwete kesho atafungua mkutano utakaohusisha wadau wa sheria kutoka ndani na nje ya sheria utakaofanyika Dar es Salaam.  Alisema wananchi wana jukumu la kutoa michango kwa tume hiyo kila wanapobaini sheria ambazo hazifai ili zifanyiwe marekebisho.
“Hizi ni sheria za wananchi hivyo wananchi wasikae mbali na tume yao, watoe mapendekezo yao ili yafanyiwe kazi kwa lengo la kuboresha,” alisema Jaji Mujulizi.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni